MBALI na kukunja mkwanja mrefu kutokana na nafasi ambayo utamaliza kwenye Ligi Kuu Bara ambayo ina ushindani mkubwa msimu wa 2024/25 kuna vita nyingine kubwa inaendelea kwa upande wa wachezaji kupambania kuandika rekodi zao.
Ipo wazi kwamba kwa msimu wa 2023/24 eneo la utupiaji vita kubwa ilikuwa kwa miamba wawili mmoja kutoka Yanga inayodhaminiwa na SportPesa mwingine Feisal Salum kutoka Azam FC ila kwa sasa Seleman Mwalimu wa Fountain Gate inayodhaminiwa na SportPesa ni namba moja.

Mwisho ni Aziz Ki alishinda vita hiyo kwa kuwa mfungaji bora na aliibuka kwenye kikosi bora akasepa na tuzo ya mchezaji bora wa msimu wa 2023/24 na Yanga walitwaa ubingwa zama za Miguel Gamondi.
Ni mabao 21 alitupia Aziz Ki na Feisal Salum wa Azam FC aliyefunga msimu na mabao 19.Katika mabao aliyofunga Ki alitupia jumla ya mabao 17.
Feisal Salum wa Azam FC yeye ujanja wake haukuwa mwingi kwenye mguu wa kushoto ambapo alifanikiwa kufunga jumla ya mabao 4. Aliachwa kwa idadi ya mabao 13 na mshindani wake Aziz.
KULIA
Kila mbabe ana mbabe wake ipo hivyo, kwenye eneo la mguu wa kulia hapa Feisal alikuwa namba moja alipofunga mabao 13.
Wakati Feisal akifunga mabao hayo 13 Aziz Ki ni mabao matatu alifunga. Alikuwa tofauti ya mabao 10 kwa upande wa mguu wa kulia ambao ulikuwa na nguvu kwa kiungo wa Azam FC, Feisal.
NDANI YA 18
Hapa wote walikuwa wakali wakiwa ndani ya 18 lakini Feisal alikuwa na hatari zaidi ambapo alifunga jumla ya mabao 17 akiwa kwenye eneo hilo.
Aziz Ki yeye alifunga jumla ya mabao 15 akiwa ndani ya 18. Hivyo alizidiwa mabao mawili pekee kwenye ukali wa kutupia mabao ndani ya 18.
NJE YA 18

Aziz Ki alitupia mabao sita akiwa nje ya 18. Miongoni mwa timu aliyofunga akiwa nje ya 18 ilikuwa dhidi ya Tabora United alipofunga bao lake la 10 ndani ya ligi ilikuwa kwa pigo huru akitumia mguu wake wa kushoto. Mwamba Feisal alitupia mabao mawili akiwa nje ya 18. Bao lake la19 la kufungia msimu alipachika akiwa nje ya 18 dhidi ya Geita Gold. Kwa upande wa pasi za mabao Aziz alitoa pasi 8 na Feisal pasi 7.
VITA IMEANZA UPYA
Tayari kila mchezaji ameanza kufanya yake ndani ya timu kwenye mechi za ushindani ikiwa ni vita imeanza upya katika msako wa ushindi uwanjani na kusaka rekodi mpya huku kasi ya Aziz Ki ikiwa ni kwenye pasi za mwisho ambapo ametoa jumla ya pasi tatu na amefunga bao moja.
Kinara kwenye utupiaji ni Suleiman Mwalimu ambaye ni mzawa katupia mabao 6 kibindoni anafuatiwa na Jean Ahoua wa Simba mwenye mabao matano na pasi nne za mabao.
Elvis Rupia wa Singida Black Stars ni mabao matano katupia akitupia matatu kwa mapigo ya vichwa. Huyu amekuwa imara katika kukaa kwenye nafasi na pacha yake na Ande Koffi imekuwa ikijibu kwenye mechi za ushindani.

HUYU HAPA RUPIA
“Wakati nakuja Tanzania kwa mara ya kwanza nilidhani ligi itakuwa ya kawaida tu, lakini baada ya kuanza kucheza nikatamani kukimbia nirudi kwetu (Kenya). Ile miezi 6 ya mwanzo ilikuwa migumu sana lakini ilinikomaza na kunijenga.”
HAWA MWENDO WA NNENNE
Edger William kutoka Fountain Gate yupo kwenye orodha hii mwingine ni Yacouba Sogne wa Tabora United, Peter Lwasa wa Kagera Sugar, Nassoro Saadun wa Azam FC, Paul Peter wa Dodoma Jiji, Offen Chikola wa Tabora United na Feisal Salum wa Azam FC.
FEISAL ANAKUJA MDOGOMDOGO

Kiungo wa Azam FC, Feisal anakuja mdogomdogo kwenye vita yake kutokana na kasi yake kuzidi kuwa imara taratibu akiwa ni namba moja kwa wakali wa kutengeneza pasi za mwisho na amebakiza pasi mbili pekee kuvunja rekodi yake ya msimu wa 2023/24.
Rekodi zinaonyesha kuwa ametoa jumla ya pasi tano na msimu wa 2023/24 alitoa jumla ya pasi 7 na mabao ametupia manne kwenye ligi hivyo bado anatafuta rekodi yake ya mabao 19 aliyofunga ndani ya ligi ambayo ina ushindani mkubwa.

