JEAN Ahoua kiungo wa Simba ameandika rekodi ya kuwa mkali kwenye mapigo ya penati ndani ya msimu wa 2024/25 akiwa katupia jumla ya mabao 10 sawa nan amba ya jezi yake inayomtambulisha akiwa na uzi wa timu hiyo huku akifunga nusu ya mabao hayo kwa mapigo ya penati.
Ahoua kafunga mabao matano kwa mapigo ya penati na mchezo dhidi ya Namungo uliochezwa Februari 19 2025 wakati ubao wa Uwanja wa Majaliwa ukisoma Namungo 0-3 Simba, penati mbili alifunga dakika ya 45 na 71 hivyo katika penati 10 ambazo Simba wamepiga ni tano alipiga Ahoua zote akifunga tano Leonel Ateba alikosa moja dhidi ya Namungo.

Simba inayonolewa na Kocha Mkuu, Fadlu Davids inafikisha pointi 50 kwenye ligi baada ya kucheza mechi 19 nafasi ya kwanza ni Yanga inayodhaminiwa na SportPesa ikiwa na pointi 52 baada ya kucheza mechi 20 ndani ya uwanja kwenye mechi za ushindani.
Mbali na kuongoza ligi, Yanga safu yao ya ushambuliaji ni namba moja ikiwa imetupia mabao 50 na katika hayo sita ni kwa penati ambapo Aziz Ki alifunga nne akikosa penati mbili na Pacome alipiga penati moja ambayo ilizama nyavuni.
MWAMBA FADLU MSIKIE
Fadlu kocha wa Simba ameweka wazi kuwa wanatambua ushindani uliopo ndani ya ligi kwa kila timu kupambana kusaka pointi tatu jambo ambalo wanalifanyia kazi kwenye mechi ambazo wanacheza uwanjani.
“Kila timu inapambana kutafuta matokeo ndani ya uwanja, kikubwa ni kuona kwamba tunapata pointi tatu muhimu na kila mchezaji anatambua majukumu yake ninawapongeza kwa namna ambavyo wanajituma.
“Mechi ambazo tunacheza ni ngumu kwa kuwa kila timu inahitaji ushindi tunaona namna ilivyo kwenye eneo la uwanja na makosa ambayo yanatokea tunafanyia kazi kwenye eneo la mazoezi ili kuwa bora zaidi.”
KITUO KINACHOFUATA MZIZIMA DABI
Mchezo unaofuata kwa Simba ni Mzizima Dabi itakuwa dhidi ya Azam FC unatarajiwa kuchezwa Uwanja wa KMC Complex unatarajiwa kuchezwa Februari 24 2025 ambapo viingilio kwenye mchezo huo ni 20,000 mzunguko na 30,000 VIP A. Ambapo zinatarajiwa kuwa dakika 90 zamoto ndani ya uwanja.

Ikumbukwe kwamba kwenye mchezo wa mzunguko wa kwanza baada ya dakika 90 ubao ulisoma Azam FC 0-2 Simba na mshambuliaji Ateba alifungua kurasa za mabao akiwa na uzi wa Simba ndani ya mechi za ligi hivyo mchezo ujao utakuwa ni kisasi kwa Azam FC wakisaka pointi tatu na Simba wakiwa na hesabu za kulinda rekodi yao.
Kwenye msimamo Simba ni nafasi ya pili ikiwa na pointi 50 inakutana na Azam FC iliyo nafasi ya tatu na pointi 43 baada ya kucheza mechi 20.
HAWA HAPA NA PACHA YAO MATATA
Pacha ya kiungo mshambuliaji Ahoua na beki Shomari Kapombe inaendelea kujengwa kwenye eneo la kucheka na nyavu ambapo Kapombe ni mtengeneza mipango mkali kuelekea kwa Ahoua.

Kwenye mabao 10 ambayo Ahoua kafunga akiwa katengeneza pasi 5 za mabao, alifunga bao moja dhidi ya JKT Tanzania kwa pigo la penati dakika ya 90 msababishaji alikuwa ni Kapombe mchezo uliochezwa Uwanja wa KMC, Complex, mabao mawili dhidi ya Namungo ya penati zote zilisababishwa na Kapombe.
Ukiweka kando mchezo huo Kapombe alitoa pasi ya bao mchezo dhidi ya Tanzania Prisons mpachikaji alikuwa ni Ahoua ambaye alipachika bao la uongozi kwenye mchezo uliochezwa Uwanja KMC Complex likiwa ni bao lake la 8 ndani ya ligi. Rekodi zinaonyesha kuwa Ahoa kafunga mabao 10 yote akitumia mguu wa kulia.
MWAMBA HUYU KUONGEZEWA MKATABA
Wakati Simba ikiwa inapambana kutwaa ubingwa wa ligi ulio mikononi mwa Yanga inayodhaminiwa na SportPesa inatajwa kuwa beki Che Malone ameitwa mezani ili kuongeza mkataba wake kuendelea kuwa Msimbazi.

Raia huyo wa Cameroon ni chaguo la kwanza la kocha Fadlu akiwa amecheza jumla ya mechi 18 akikomba dakika 1,620 huyu ni mfungaji wa bao la kwanza la Simba kwenye ligi msimu wa 2024/25 ilikuwa Uwanja wa KMC, Complex Agosti 18 2024 dhidi ya Tabora United dakika ya 13.
Taarifa zinaeleza kuwa mabosi wa Simba wameanza kufanya naye mazungumzo beki huyo ili kuongeza kandarasi mpya kuitumikia Simba ambapo kuna vipengele vimewekwa.

