
WAKIWA nchini Afrika Kusini, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Bara, Yanga leo Jumamosi jioni wanatarajia kuvaana na FC Ausburg kutokea nchini Ujrerumani katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki.
Mchezo huo unatarajiwa kupigwa kwenye dimba la Mbombela kuanzia majira ya saa 9:00 alasiri kwa saa za Afrika Kusini, ambayo ni sawa na saa 10:00 kwa saa za Tanzania.
Taarifa ambazo zimeripotiwa na Yanga ni kuwa mchezo huo ni wa mashindano ya Kombe la Mpumalanga ambapo Yanga wamealikwa kushiriki.
Wakiwa nchini Afrika Kusini, Yanga wanatarajiwa kucheza mechi tatu za kirafiki ambapo pia watashiriki mashindano ya Kombe la Toyota huku miongoni mwa timu watakazovaana nazo ni Kaizer Chiefs ya kocha Nasreddine Nabi.
MSAFARA WA YANGA

Yanga Alhamisi ya wiki hii rasmi kikosi chao kilikwea pipa kwenda Afrika Kusini kwa ajili ya ratiba hiyo ya michezo ya kirafiki.
Kikosi cha Wananchi ambacho kinadhaminiwa na Kampuni ya michezo ya Kubashiri ya SportPesa kimelazimika kukatisha kambi yake ya maandalizi ya kabla ya msimu ‘Pre-season’ ambayo ilikuwa ikiendelea Avic Town, Kigamboni Dar es Salaam.
Msafara wa wachezaji wa Yanga waliosafiri ni kama ifuatavyo;
Makipa
Djigui Diarra
Aboutwalib Mshery
Khomeiry
Walinzi
Bakari Mwamnyeto
Ibrahim Bacca
Dickson Job
Yao Attohoula Kouasi
Nickson Kibabage
Chadrack Boka
Kibwana Shomari
Viungo
Khalid Aucho
Salum Abubakar
Jonas Mkude
Mudathir Yahya
Maxi Nzengeli
Aziz Andembwile
Viungo washambuliaji
Stephane Aziz Ki
Farid Mussa
Denis Nkane
Clatous Chama
Duke Abuya
Washambuliaji
Clement Mzize
Kennedy Musonda
Prince Dube
Jean Baleke (Anasubiri kutambulishwa)
KAMWE ATANGAZA YANGA KURUDI NA UBINGWA

Akizungumzia safari yao Ofisa habari wa timu hiyo, Ali Kamwe alisema: “Ukubwa wa timu yetu ndio umeifanya leo hii tumepata mialiko mikubwa nje ya Tanzania ambapo tunakwenda kucheza michezo ya kirafiki.
“Michezo hii kwetu ni sehemu ya maandalizi ya Kampeni yetu kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao ambapo malengo yetu makubwa ni kuhakikisha tunaandika rekodi ya kufika mbali katika mashindano hayo na ikiwezekana kushinda ubingwa.
“Kikosi chote kinasafiri na timu kwa ajili ya maandalizi ya mchezo huu, wakiwemo wachezaji wetu wapya ambao ni sehemu ya maboresho ya kikosi chetu kuelekea msimu ujao wa 2024/25.
“Tumewaambia waliotualika waandae utaratibu mzuri kwetu kwa ajili ya kurudi na kombe letu.”
ISHU YA BALEKE YANGA IKOJE?
Akizungumzia sakata la Baleke, Ally Kamwe alisema: “Baleke hatujamtambulisha hivyo huenda watu wakawa wanamfananisha, lakini kuna mchezaji tutamtangaza lakini sio kwa sasa hatuna la kusema kuhusu mchezaji huyo, tunaomba muwe na subira.”
Wakiwa nchini Afrika Kusini Yanga wanatarajiwa kucheza michezo mitatu ya kirafiki ambapo miongoni mwa timu watakazovaana nazo ni Augsburg kutokea nchini Ujerumani.
Mwaliko wa Yanga ni kutoka ndani ya kikosi cha timu ya Kaizer Chiefs ambao wamekuwa na mahusiano nao ya ukaribu katika masuala ya kiuongozi na uendeshaji wa klabu.
Msimu uliopita Kaizer Chiefs walialikwa na Yanga kwa ajili ya mchezo wa kirafiki wa kuadhimisha kilele cha wiki ya Wananchi, mchezo ambao ulipigwa kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.
TAWI LA YANGA SAUZ
Unaweza kusema licha ya ugeni wao wakiwa nchini Afrika Kusini, Wananchi wanatarajia maisha ya uenyeji kwani ikumbukwe msimu uliopita walifanikiwa kuanzisha Tawi jipya linalofahamika kama ‘Tawi la Yanga Afrika Kusini’.
Hii ni wakati timu hiyo ilipoenda kuvaana na Mamelodi Sundowns Ijumaa ya Aprili 5, mwaka huu katika mchezo wa marudiano wa Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu wa 2023/24 ambapo Yanga waliingia katika mchezo huo wakiwa na kumbukumbu ya matokeo ya suluhu katika mchezo wa mkondo wa kwanza uliopigwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.
INJIA HERSI ATOA TAMKO

Kufuatia tukio hilo, Rais wa timu hiyo Injina Hersi Said alisema: “Niweke rekodi sawa, sisi tuna matawi lukuki nje ya mipaka ya Tanzania. Kwa Mfano kule Marekani tunalo tawi la uanachama. Tunasisitiza mashabiki wetu nje ya Tanzania kutumia fursa hii ya kufungua account ya Tanzanite ya CRDB ambapo imetufanya kuwa karibu sana Wanachama wetu wa diaspora.
“Niwapongeze sana idara ya habari na Wanachama kwa kuweka mipango mikakati madhubuti ya kampeni ya ‘Twenzetu kwa Madiba’. Ama kwa hakika idara hizi mbili zina watu wenye upeo mkubwa wa maarifa wa kuanzisha agenda zenye dhima kwa Klabu.
“Nichukue nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza sana mashabiki wa wetu hapa Afrika Kusini na pia niwashukuru wadhamini ambao wamedhamini safari yetu ya Afrika Kusini.

