- Tatu kutoka Ligi Kuu Tanzania Bara kutazama fainali Muungano Cup 2025 jukwaani
- Azam FC kilichowatuliza Singida Black Stars nao kimewamaliza jumlajumla
- JKU SC sio wa mchezomchezo wanagawa dozi bila idadi kwa wapinzani wao
YANGA SC inayoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara ina kibarua cha kusaka tiketi kutinga hatua ya kutinga fainali Muungano Cup itakapokaribishwa na Zimamoto FC.

Ni Aprili 29 2025 mchezo huo unatarajiwa kuchezwa Uwanja wa Gombani saa 1:15 Pemba kwa kila timu kusaka ushindi kutinga hatua ya fainali kukabiliana na wababe JKU SC.
Moto wa JKU SC haupoi kwenye Muungano Cup kwa kuwa wababe wote wanaoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara ambayo ni namba nne kwa ubora Afrika walipokutana naye walipoteza mazima.
HESABU ZA ZIMAMOTO KUFIKA NUSU FAINALI
Kete ya kwanza kwenye robo fainali ya Zimamoto ilikuwa ni Aprili 25 2025 ilipata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Coastal Union inayoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara. Kwenye mchezo huo bao pekee la ushindi lilifungwa na Rashid Salum dakika ya 28.
Bao hilo lilidumu mpaka mwisho wa mchezo na Coastal Union ikawa imegota mwisho katika Muungano Cup 2025. Nyota Rashid Salum wa Zimamoto kwenye mchezo huo wa hatua yar obo fainali alitwaa tuzo ya mchezaji bora.
SAFARI YA YANGA ROBO FAINALI
Kutoka Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga SC ilipata ushindi kwenye mchezo wao wa hatua ya robo fainali dhidi ya KVZ FC baada ya dakika 90 wakawafungashia virago wapinzani wao hao ndani ya uwanja.

Ni Aprili 26 2025 siku ya Muungano Yanga SC ilipata ushindi wa mabao 2-0 ni Aziz Ki alipachika bao la ufunguzi dakika ya 29 kwenye mchezo uliochezwa Uwanja wa Gombani.
Bao la pili kwenye mchezo huo ni mali ya Dennis Nkane ambaye alianzia benchi alipachika bao hilo dakika ya 85 zikiwa zimesalia dakika 5 mpira kugota mwisho.
Kwenye mchezo huo kiungo Mudathir Yahya alichaguliwa kuwa mchezaji bora ambaye Aprili 29 2025 anatarajiwa kuwa kwenye kazi dhidi ya Zimamoto katika msako wa ushindi.
AZAM FC MWENDO WAMEUMALIZA
Matajiri wa Dar, Azam FC mwendo wameumaliza kwenye Muungano Cup 2025 kwa kufungashiwa virago na JKU SC kwenye mchezo uliochezwa Uwanja wa Gombani, Pemba Aprili 28 2025.

Inakuwa ni timu ya pili inayoshiriki Ligi Kuu Bara kuumaliza mwendo mbele ya JKU SC amabayo itakuwa jukwaani kumsubiri mshindi wa mchezo kati ya Zimamoto FC ama Yanga SC kucheza naye hatua ya fainali.
Walianza na Singida Black Stars katika hatua ya robo fainali Aprili 24 ilikuwa JKU SC 2-2 Singida Black Stars katika penalti ilikuwa JKU SC 6-5 Singida Black Stars mwendo ukagota mwisho.
Aprili 28 2025, Azam FC waliumaliza mwendo kwa kushuhudia ubao wa Uwanja wa Gombani ukisoma JKU SC 2-1 Azam FC. Dakika 90 zilikuwa kicheko kwa JKU SC na maumivu kwa Azam FC.
Licha ya Azam FC kuanza kufunga mapema dakika ya 15 kupitia kwa Yeison Fuentes bao hilo liligotea dakika ya 50 kwa wapinzani wao kuweka usawa na kuongeza bao la ushindi katika dakika ya 85.
Neve Adelin alipachika bao la kusawazisha kwenye mchezo huo dakika ya 50, bao la ushindi likafungwa na Fredy Seleman dakika ya 80 likiwapa tiketi kutinga hatua ya fainali.
JKU SC anamsubiri mshindi wa mchezo wa leo kati ya Zimamoto vs Yanga saa 1:15. Kwa timu ambazo zinashiriki Ligi Kuu Tanzania Bara ni tatu zimeondolewa ambazo ni Coastal Union, Singida Black na Azam FC kutoka Ligi Kuu Bara
HIZI HAPA TIMU ZILIZOTOLEWA NA JKU SC
Singida Black Stars kwenye msimamo wa ligi ipo nafasi ya nne imekusanya jumla ya pointi 53 baada ya mechi 27. Ni ushindi kwenye mechi 16, sare 5 ikipoteza jumla ya mechi 6.
Safu ya ushambuliaji ya Singida Black Stars ni mabao 40 imetupia na ukuta ukiruhusu mabao 21 msimu wa 2024/25.
AZAM FC
Wababe hawa waliopo nafasi ya tatu walikutana na balaa la JKU SC. Pointi za oni 54 baada ya mechi 27, ushindi kwenye mechi 17, sare 6 na walipoteza mechi tano msimu wa 2025.

