
LEO Jumatano kikosi cha Simba kinatarajiwa kushuka uwanjani kuvaana na kikosi cha KVZ katika mchezo wa nusu fainali ya kwanza ya michuano mipya ya Kombe la Muungano.
Mchezo huo unatarajiwa kupigwa kuanzia saa 2:15 usiku kwenye Uwanja wa New Amaan Complex.
MSAFARA WA SIMBA ZANZIBAR

Kikosi cha wachezaji 26 wa Simba AMBAYO IMEWAHI KULAMBA dili la Kampuni ya Michezo ya SportPesa, benchi la ufundi pamoja na Viongozi wao jana Jumanne waliwasili visiwani Zanzibar tayari kwa ajili ya mashindano hayo mara baada ya kuondoka Dar es Salaam majira ya saa sita mchana.
KUHUSU MICHUANO YA KOMBE LA MUUNGANO
Michuano ya Muungano imerejea baada ya kupita miaka 20, ambapo kwa msimu huu inatarajiwa kushirikisha timu nne, mbili kutoka Tanzania Bara na nyingine mbili kutoka Zanzibar.
MAKUNDI YA MASHINDANO HAYO
Katika mashindano hayo Simba wamepangwa kucheza na KVZ katika mchezo wa nusu fainali ya kwanza ambao utapigwa leo Jumatano saa 2:15 usiku katika Uwanja wa New Amaan Complex.
Mshindi wa mchezo huo wa Nusu Fainali ya kwanza anatarajiwa kukutana na mshindi wa nusu fainali ya pili ambayo inatarajiwa kuwakutanisha Azam FC dhidi ya KMKM ambao watakutana kesho Alhamisi saa 2:15 katika dimba hilo hilo la New Amaan Complex.
Simba wanaingia katika mashindano hayo wakiwa na kumbukumbu mbaya ya kipigo cha mabao 2-1 katika mchezo wao dhidi ya watani wao wa jadi Yanga, ambao ulipigwa kwenye Uwanja wa wa Benjamin Mkapa.
Katika mchezo huo uliopigwa Aprili 20, mwaka huu ni nyota raia wa Burkina Faso, Stephanie Aziz Ki aliyeipa bao la kwanza dakika ya 18 kwa mkwaju wa penati, baada ya yeye mwenyewe kufanyiwa madhambi ndani ya 18.
Baada ya bao hilo Simba waliongeza kasi ya kutaka kusawazisha, huku tukitengeneza nafasi kadhaa za kufunga lakini tulipoteza umakini.
Straika mpya wa Yanga, Joseph Guede aliwapatia Yanga bao la pili dakika ya 39 baada ya kuwazidi ujanja walinzi wa Simba katika tukio ambalo walinzi wa Simba walitaka kutega mtego wa kuotea.
Simba walipata bao lao pekee la kufutia machozi dakika ya 74 ya mchezo baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa Clatous Chama.
VIKOSI VYA KARIAKOO DABI

Kwa upande wa Yanga kikosi kilichoanza mchezo wa Jumamosi ni kama ifuatavyo: Diarra, Yao, Lomalisa (Kibabage 12′), Bacca, Job, Aucho, Nzengeli (Mkude 85′) , Mudathir (Okra 85′), Guede, Aziz Ki, Mzize
Kupitia mchezo huo nyota wanne wa Yanga walionyeshwa kadi za njano kwa mchezo usio wa kiungwana ambao ni: Job, Mudathir 27′ Aucho, Guede 90+4
Kwa upande wa Simba kikosi kilichoanza mchezo huo ni:
Lakred, Israel, Zimbwe Jr, Che Malone Henock (Kazi 15′), Babacar (Mzamiru 75′), Kibu (Jobe 75′), Ngoma (Miqussone 57′), Kanoute, Saido (Freddy 57′), Chama.
Kwa upande wa Simba ni nyota watatu pekee ndio Walionyeshwa kadi za njano kwa mchezo usio wa kiungwana ambao ni: Chama 56′ Babacar 65′ Mzamiru 90+6
AHMED ATOA TAMKO ZITO

Akizungumzia mwenendo wao wa kusuasua, Meneja wa habari na mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally amesema: “Dhahabu hupitishwa kwenye moto mkali ili ipate thamani na iwe bora.
“Licha ya kuwa huteseka inapopita kwenye moto huo lakini mwishoe hubaki safi, bora na thamani yake huongezeka maradufu. Wana Simba tuvumilie kupita kwenye moto huu mkali ili tuwe bora na hadhi yetu irejee.
“Najua maumivu ni makubwa kwa kua moto ni mkali, lakini hatuna budi kuvumilia kwani ndio njia pekee ya kurudi kwenye thamani yetu.”
Kuhusu mashindano ya Kombe la Mapinduzi Ahmed amesema: “Tumewasili Visiwani Zanzibar kwenye majukumu mapya ya kombe la Muungano. Mechi yetu ya kwanza ni leo April 24 Saa 2:15 Usiku dhidi ya KVZ.”

