KIKOSI cha Simba tayari kimewasili na kuanza rasmi mazoezi kwenye kambi yao fupi visiwani Zanzibar kwa ajili ya kujiandaa na mchezo wa Dabi ya Kariakoo dhidi ya Yanga.

MOTO KUWAKA JUMAMOSI APRILI 20, KWA MKAPA

Mara baada ya mchezo wa sare ya bao 1-1 dhidi ya Singida Black Stars, Simba kwa mara nyingine watashuka uwanjani kuvaana na Yanga kwenye mchezo ambao umepangwa kupigwa Aprili 20, mwaka huu kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.
MARA YA MWISHO WALIKUFA 5-1

Ikumbukwe mara ya mwisho timu hizo kukutana katika mchezo wa mkondo wa kwanza uliopigwa Novemba 5, mwaka jana Simba ambao wamewahi kulamba dili la udhamini wa Kampuni SportPesa, walikubvali kipigo cha fedheha cha mabao 5-1 kutoka kwa watani zao hali iliyopelekea taharuki kubwa na kuwajibishwa kwa baadhi ya watendaji wa timu hiyo akiwemo aliyekuwa kocha Mkuu Mbrazili, Robert Olivieira.
BINGWA KUAMULIWA JUMAMOSI?
Achana na matokeo ya mchezo wa mkondo wa kwanza kwa kipigo cha Simba cha mabao 5-1 ambayo yanaathiri mchezo huu wa Jumamosi, lakini mchezo huu unazidi kuwa mgumu kutokana na takwimu za vita ya ubingwa kwa timu nzote mbili.
Mpaka sasa Yanga wanaongoza ligi kwa tofauti ya pointi 9 dhidi ya Mnyama licha ya kwamba Yanga wamecheza mchezo mmoja zaidi, hivyo ikiwa wataibuka na ushindi katika mchezo wa Jumamosi basi Yanga watakuwa wameizidi Simba pointi 12 kabla ya viporo, hivyo kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kutangaza ubingwa wa tatu mfululizo.
Kwa upande wa Simba ni lazima kuhakikisha wanashinda mchezo huo ili kupunguza wingi wa pointi wanazozidiwa na Yanga na kuurejesha matumaini ya mbio za ubingwa.
ALICHOSEMA MENEJA WA SIMBA AHMED ALLY

Meneja Habari na Mawasiliano wa timu hiyo, Ahmed Ally amesema kikosi kimeondoka kwa ajili ya kuweka fupi kujiandaa na mchezo huo wa Jumamosi huku akiweka wazi kuwa wamejipanga kusaka matokeo.
Ahmed amesema kambi hiyo ya Zanzibar itahusisha wachezaji wote walio kwenye mpango wa kocha mkuu Benchikha, isipokuwa wale ambao watakuwa na ruhusa maalum.
“Kikosi chetu kimewasili Zanzibar kwa ajili ya kuweka kambi fupi ya kujiandaa na mchezo wetu dhidi ya Yanga.
“Kambi hii ya Zanzibar itahusisha wachezaji wote walio kwenye mpango wa kutumika na mwalimu na hii inafanyika ili kumpa nafasi kocha kufanya maandalizi ya kutosha kutokana na ukubwa wa mechi,” Amesema Ahmed.
Uongozi wa timu hiyo umeweka wazi kuwa utaingia katika mchezo huo wakiwa na kiu kubwa ya kuibuka na ushindi licha ya kwamba wanafahamu Yanga wamekuwa kwenye kiwango bora kwa sasa.
YANGA KICHEKO, SIMBA KUJIULIZA UPYA
Yanga wataingia katika mchezo huu wakiwa na ari zaidi nkufuatia kuwa na mfululizo ya matokeo mazuri, huku Simba wakiichukua nafasi hii kujiuliza upya baada ya kuwa wanapitia kipidi kigumu katika siku za karibuni.
Kipindi kigumu wanachopitia Simba kimewafanya wacheze michezo minne mfululizo katika mashindano yote bila kupata matokeo ya ushindi.
Michezo hiyo minne ambayo Simba hawajapata ushindiu ni dhidi ya Singida Black Stars, Mashujaa na michezo miwili ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al Ahly.
AHMED AWAITA MASHABIKI
Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed amewaomba mashabiki kujitokeza kwa wingi katika mchezo huo kwa ajili ya kuisapoti timu huku akiahidi nao wanaahidi kuwalipa furaha.
Ahmed amesema anajua mashabiki hawana furaha hasa baada ya timu kupitia kipindi kigumu.
“Tunawaomba mashabiki wetu wajitokeze kwa wingi, tunajua wameumizwa na matokeo yetu ya mechi zetu zilizopita lakini tumejipanga, tunawaahidi tutawapa furaha,” amesema Ahmed
ZEGE HALILALI HUKO SIMBA
Licha ya changamoto za uchovu wa safari, mastaa wa Simba zege halilali ndivyo unavyoweza kusema kwani walifikia na kuanza progamu za mazoezi mara moja, ambapo mastaa mbalimbali walionekana wakijifua vikali kujiandaa na mchezo huo wa Jumamosi.
